Alhamisi , 6th Oct , 2016

Waandishi wa Habari nchini wametakiwa kuusoma na kuuelewa vyema muswada sheria ya huduma ya vyombo vya habari 2016, uliowasilishwa na serikali bungeni, kwa ajili ya kuutolea maoni.

Rais wa Muungano wa Klabu za Waandishi wa Habari nchini UTPC, Deo Nsokolo, akifungua Mkutano Mkuu wa Wanachama wa Klabu za Waandishi wa Habari nchini UTPC unaofanyika Jijini Mwanza kwa siku mbili, kuanzia leo Oktoba 06,2016.

Hayo yamesemwa leo Mkoani Mwanza na Rais wa Muungano wa Klabu za Waandishi wa Habari nchini UTPC, Deo Nsokolo, wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Wanachama wa klabu hizo unaofanyika Jijini Mwanza kwa siku mbili, kuanzia leo Oktoba 06,2016.

Nsokolo amesema tayari kamati ya bunge imekwisha kabidhiwa muswada huo kwa ajili ya kukusanya maon hivyo ni vyema waandishi wa habari ambao wanaguswa moja kwa moja na muswada huo, wakausoma kiundani na kisha kutoa maoni yao kabla ya kuwasilishwa bungeni ili kuidhinishwa.

Muswada huo uliwasilishwa Bungeni na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Nape Nnauye, ambapo alieleza kuwa kupitishwa kwake kutasaidia kuleta mageuzi makubwa ya kitaaluma kwa wanahabari pamoja na huduma za vyombo vya habari nchini.