Jumamosi , 29th Aug , 2015

Mashindano ya Dance 100% 2015 hatua ya Robo Fainali hatimaye yamekamilika na kufanikisha kupatikana kwa makundi 10 ambayo yanasonga mbele kulekea hatua ya fainali ya mashindano hayo makubwa Afrika Mashariki.

Washindi katika picha ya pamoja

Kutokana na uwezo mkubwa walioonesha mbele ya majaji Majokery, Wazawa Crew, The Best, Cute Babies, Best Boys Kaka Zao, The Winners, Team ya Shamba, The WD, Team Makorokocho na Quality Boys ndio makundi yaliyofanikiwa kuingia nusu fainali.

Upekee na mvuto wa aina yake kutoka kwa mashabiki kati ya mambo mengine ulikuwa ni muonekano mpya ya set ya jukwaa la madansa jipya kabisa ambalo lipo juu lililowezesha kila aliyeweza kufika kujionea burudani ya dansi na ubunifu katika hali ya kipekee.

Kwa kipekee pia na kwa tathmini ya majaji, Kundi la Majokery ni kati ya washindani waliomwagiwa sifa nyingi kwa kuzingatia kuhusisha nyimbo za kitamaduni katika dansi yao, na vilevile usimuliaji wa hadithi kupitia kile walichokicheza.

Kama sehemu ya tathmini ya mashindano hayo, mratibu wa mashindano kutoka BASATA, Kwerugira Maregesi ametoa wito kwa makundi yaliyofanikiwa kuingia nusu fainali kuongeza mazoezi zaidi na kuzingatia vigezo vya mashindano kama siri pekee ya kuweza kushinda.

Mpango huo mzima ambao ulisimamiwa vizuri na majaji Super Nyamwela, Queen Darleen na Shetta na kushereheshwa na T Bway pamoja na Maggie Vampire, umeletwa kwako na team nzima ya East Africa Radio na East Africa TV na kudhaminiwa kwa nguvu kabisa na Coca Cola na Vodacom Tanzania.