Jumatatu , 5th Jan , 2015

CHAMA cha Riadha Tanzania RT, kimevitaka vyama vya Riadha mikoani kuandaa mashindano mbalimbali ya mikoa ili kuweza kuendeleza mchezo wa Riadha hapa nchini.

Akizungumza na East Africa Radio, Katibu Mkuu a RT, Suleiman Nyambui amesema mashindano hayo yanatakiwa kushirikisha wanafunzi kutoka shule mbalimbali za msingi na Sekondari ambao ndio chanzo cha kukuza mchezo huo.

Nyambui amesema, viongozi hao wanapoandaa mashindano hayo, wanatakiwa kushirikiana na TAMISEMI na maafisa Elimu wote wawe kitu kimoja ili kuweza kuhamasisha wanafunzi kuweza kushiriki katika michezo.

Nyambui amesema, wanaamini mashindano hayo yatasaidia kuweza kupata wanariadha bora nchini ambapo RT inatarajia kuandaa shule ambayo itasaidia vijana hao kuweza kupata mafunzo zaidi katika kuukuza mchezo huo.