Jumatano , 12th Jun , 2019

Uongozi wa klabu ya Azam FC, leo umeingia mkataba wa miaka miwili na Kocha Etienne Ndayiragije, kwa ajili ya kuinoa timu hiyo kuanzia msimu ujao.

Kocha Etienne Ndayiragije (kushoto) na Ofisa Mtendaji Mkuu, Abdulkarim Amin 'Popat.

Ndayiragije, anachukua nafasi ya makocha wazawa, Abdul Mingange na Idd Nassor Cheche, waliokuwa makocha wa muda wa timu hiyo hadi kumalizika kwa msimu uliopita baada ya kusitishiwa mkataba kwa Hans Van Der Pluijm na Juma Mwambusi.

Zoezi la kocha huyo kuingia mkataba limefanyika Ofisi za Mzizima, mbele ya waandishi wa habari, Azam FC ikiwakilishwa na Ofisa Mtendaji Mkuu, Abdulkarim Amin 'Popat' na Mratibu Phillip Alando.

Azam FC ikiwa na changamoto ya kushiriki Kombe la Shirikisho Afrika msimu ujao, imejiridhisha vilivyo hadi kumtwaa Ndayiragije kutoka KMC, kwani ana rekodi ya kuifikisha Vital'O ya Burundi hatua ya makundi mwaka 2016.

Aidha ameeleza kuwa amejipanga vilivyo kuendeleza utaratibu wa kupandisha vijana, ikiwa ndio falsafa aliyopitia pia katika timu zake za awali Mbao na KMC, alizofundisha hapa nchini.

Kocha huyo anatarajia kuanza kukinoa kikosi hicho kuanzia Juni 20 mwaka huu, Azam FC itakapoanza maandalizi ya msimu mpya na kujiandaa na michuano ya Kombe la Kagame ikiwa kama bingwa mtetezi.