Jumanne , 7th Jan , 2020

Aliyekuwa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi ametoa kauli yake kuhusu mchezo wa 'Watani wa Jadi' Simba na Yanga, ikiwa ni mwezi mmoja baada ya kurejea kutoka gerezani.

Mchezo wa Simba na Yanga

Malinzi pamoja na aliyekuwa Katibu wa shirikisho hilo, Selestine Mwesigwa walikuwa akikabiliwa na mashtaka kadhaa likiwemo la utakatishaji fedha, kabla ya kufikia mwisho mwezi Disemba 2019 kwa kupokea hukumu ya jela miaka miwili au kulipa faini ya shilingi laki 5 baada ya kukutwa na hatia, ambapo wamekubali kulipa faini.

Malinzi ameibuka hii leo katika ukurasa wake wa Twitter, ikiwa ni siku kadhaa baada ya kumalizika kwa mchezo wa Simba na Yanga, ambapo amewashukuru wadau wa soka na mitandao mbalimbali barani Afrika kwa kuutangaza mchezo huo.

Pia ametoa ushauri kuwa jambo hilo linahitajika kufanyika mara kwa mara ili kukuza ubora wa mchezo huo pamoja na mapato.

Mchezo huo wa Simba na Yanga unakadiriwa kuingiza takribani watazamaji 58,000 ikiwa ni mahudhurio makubwa zaidi ya watazamaji katika mechi ya vilabu Afrika Mashariki.