Ijumaa , 8th Dec , 2017

Daktari wa timu ya taifa ya Tanzania Bara (Kilimanjaro Stars ) Dr. Richard Yomba amethibitisha kuwa mlinzi wa timu hiyo na klabu ya soka ya Yanga Kelvin Yondani atakuwa nje ya uwanja kwa wiki mbili.

Katika taarifa iliyotolewa na klabu ya Yanga asubuhi hii  imeeleza kuwa daktari huyo amewapa taarifa kuwa Yondani amepata majeraha ya kifundo cha mguu kwenye mchezo wa jana dhidi ya Zanzibar Heroes.

Katika mchezo wa jana Kilimanjaro Stars ilikubali kichapo cha mabao 2-1 kutoka kwa Zanzibar Heroes kwenye mchezo wake wa pili kundi A michuano ya CECAFA Senior Challenge inayoendelea nchini Kenya.

Yanga pia imethibitisha kurejea kwa kiungo wake Pappy Kabamba Tshishimbi, katika kikosi kilichofanya mazoezi asubuhi ya leo kwenye uwanja wa Uhuru jijini Dar es salaam.

Kilimanjaro Stars imebakiza michezo miwili kwenye kundi A dhidi ya Rwanda na wenyeji Kenya ambapo kocha mkuu wa timu hiyo Ammy Ninje amesema bado timu hiyo ina nafasi ya kutinga nusu fainali.