Ijumaa , 24th Dec , 2021

Mabingwa watetezi wa Ligi Kuu NBC Tanzania, Klabu ya Simba inatazamiwa kuendelea na kampeni ya kuutetea Ubingwa kwa kushuka dimbani dhidi ya KMC saa 10:00 Jioni ya leo kwenye dimba la Ali Hassan Mwinyi mkoani Tabora.

(Kikosi cha Simba cha msimu wa mwaka 2021-2022)

Kuelekea kwenye mchezo huo, Kocha Msaidizi wa Simba, Hitimana Thierry amethibitisha kuwa watawakosa nyota wao watatu ilhali mshambuliaji Chris Mugalu na kiungo Larry Bwalya wamerejea kikosini.

"Tumejiandaa vizuri licha ya kuwakosa baadhi ya nyota wetu kama John Rafael Bocco, Bernard Morrison na Erasto Nyoni ambao bado wanaumwa, habari nzuri ni kurejea kikosini Rally Bwalya ambaye hakuwepo katika kikosi kilichoenda Kagera". Amesema Hitimana.

(Kutoka Kushoto: Mshambuliaji John Bocco, Beki Erasto Nyoni na Winga Bernard Morrison)

Kwa Upande Mwingine:

Meneja wa Simba, Patrick Rweyemamu amesema wachezaji 16 waliokuwa wanaumwa na mafua, homa na kifua hadi kupelekea mchezo wao dhidi ya kagera kuhairishwa siku chache zilizopita, kuwa wanaendelea vizuri na wapo tayari.

Simba ipo nafasi ya pili ikiwa na alama 18, utofauti wa alama 5 na vinara Yanga wenye alama 23. Coastal Union waliopo nafasi ya 7 ikiwa na alama 14 watawakaribisha Mbeya City waliopo nafasi ya 5 wakiwa na alama 15 mchezo utakaochezwa kwenye dimba la Mkwakwani Jijini Tanga mchezo utakaochezwa saa 10:00 Jioni.