Jumanne , 18th Dec , 2018

Klabu ya soka ya Simba kupitia kwa Afisa Habari wa klabu hiyo, Haji Manara imetaja sharti muhimu linalohitajika ili kufanikisha azma ya kuing'oa Nkana Red Devils katika hatua ya mtoano ya Klabu Bingwa barani Afrika wikiendi hii.

Haji Manara

Akizungumza katika mkutano na wanahabari, makao makuu ya klabu hiyo mtaa wa Msimbazi Jijini Dar es salaam, Manara amesema kuwa sharti hilo ni mashabiki wa klabu hiyo kwenda kwa wingi kujaza uwanja na kuisapoti timu yao.

"Naongea na mashabiki na wanachama wa Simba, kwa mechi hii tunawahitaji sana, tunahitaji tujaze uwanja. Uwanja wa taifa unachukua mashabiki kati ya elfu 57 hadi elfu 60. Tunataka tufanye kama 'Simba Day', watu wajae wakivaa jezi zao nyekundu na nyeupe, mamngoma yawepo ya kutosha pale," amesema Manara.

"Alhamisi nitakutana na wale viongozi wa vikundi vya ngoma, ili wawepo kuanzia pembe ya kwanza hadi ya mwisho na viingilio vitakuw rafiki sana ili kila mwana Simba awepo uwanjani," ameongeza.

Aidha Manara ametumia mkutano huo kutangaza viingilio vya mchezo, ambavyo ni Sh 20,000 kwa VIP A, Sh 10,000 kwa VIP B, na viti vya mzunguko ni Sh 3,000.

Simba inatarajia kucheza mchezo wa marudiano na Nkana Red Devils ya Zambia Jumapili, Desemba 23. Katika mchezo wa kwanza uliochezwa nchini Zambia, Simba ilifungwa kwa mabao 2-1, ambapo katika mchezo huo wa marudiano inahitaji bao moja pekee ili kujihakikishia nafasi ya kufuzu hatua inayofuata ya makundi.