Jumatano , 12th Mei , 2021

Ligi kuu soka Tanzania bara inaendela leo kwa michezo miwili, Mkoani Lindi Namungo watakuwa wenyeji wa Mtibwa Sugar, na Ihefu FC watakuwa wenyeji wa Polisi Tanzania Jijini huko Mbeya.

Wachezaji wa Mtibwa Sugar wakishangilia goli dhidi ya Namungo kwenye mchezo wa mkondo wa kwanza

Katika dimba la Majaliwa Ruangwa Lindi wauaji wa kusini Namungo FC wanaoshika nafasi ya 11 wakiwa na alama 32 watakuwa wakiutafuta ushindi wa kwanza baada ya kucheza michezo mitatu ya Ligi Kuu pasiko kushindi mchezo hata mmoja, katika michezo hiyo wamefungwa michezo 2 na wametoka sare mchezo mmoja.

Wakati wapinznaia wao wa jioni ya leo Mtibwa Sugar nao wana hali mbaya wapo nafasi ya 17 wakiwa na alama 28 na wameshinda mchezo mmoja tu kwenye michezo mitano ya mwisho ya Ligi Kuu. Mchezo wa mkondo wa kwanza timu hizi zilipokutana Mtibwa waliibuka na ushindi wa bao 1-0.

Kule Mbarali Mbeya, Ihefu FC watakipiga dhidi ya Polisi Tanzania na tofauti ya timu hizi kwenye msimamo ni alama saba (7) Polisi wapo juu wakiwa na alama 37 wakiwa nafasi ya nane (8) wenyeji Ihefu wapo nafasi ya 16 wakiwa na alama 30.

Mchezo wa mkondo wa kwanza ulimalizika kwa sare ya bila kufunga, mchezo wa jioni ya leo kati ya timu hizi itakuwa ni kwa mara ya pili timu hizi zinakutana kwenye michezo ya ligi kuu. Micheo yote miwili ya leo inachezwa Saa 10:00 Jioni