Tuesday , 1st Nov , 2016

Shirika la Umoja wa Mataifa linalojishugulisha na idadi ya watu dunia (UNFPA) Tanzania imeishauri nchi za Afrika kutoa kipaumbele kwenye masuala ya elimu na afya ya uzazi hasa kwa wasichana wa kike wa umri wa miaka 10 kwa sasa.

Upasuaji katika harakati za kuokoa vifo vitokanavyo na uzazi

Limesema hiyo itasaidia kuwa na wazalishaji bora ifikapo mwaka 2030 ambapo malengo endelevu yatafikia tamati.

Mratibu wa shirika hilo nchini Bw. Warren Brighton amesema hayo leo jijini Dar es Salaam katika mkutano uliokutanisha nchi zaidi ya 12 za Afrika Mashariki na Kati, na kueleza kuwa bila kuwekeza kwa watoto wa kike leo, suala la vifo vitokanavyo na uzazi halitaepukika hivyo jamii kuendelea kuteseka na vifo vya mama na mtoto na kuwa na vijana wasiochangia kwenye uchumi wa nchi.

Naye Mratibu wa Shirika la UNFPA nchini Kenya Bw. Douglas Waudo amesema asilimia 50 ya vifo vya mama na mtoto nchini Kenya vinatokea zaidi kwenye maeneo yenye elimu duni na vituo vya afya vyenye upungufu mkubwa wa maabara hivyo kuzihimiza nchi za Afrika kuwekeza zaidi kwa watoto wa kike.