Wednesday , 19th Dec , 2018

Kampuni ya filamu ya Disney ambayo hutengeneza filamu ya 'The Lion King', inapitia wakati mgumu kutoka kwa raia mbalimbali barani Afrika, wakitaka kampuni hiyo kuacha kutumia neno 'Hakuna Matata' kama chata yao ya kibiashara.

Mjadala huo umeanzishwa na raia wa Zimbabwe, Shelton Mpala,ambaye amewataka Waafrika kusaini na kupinga kitendo cha kampuni ya Disney kutumia msemo huo kama alama yao ya kibiashara kwenye filamu ya The Lion King, ambayo wanatarajia kuitoa tena mwaka 2019 ikiwa imeboreshwa.

Mzimbawe huyo amesema kitendo cha Walt Disney kutumia 'Hakuna Matata' kama alama yao ya kibiashara, ni ukoloni na unyonyaji, kitendo ambacho kimeonekana kuungwa mkono na Waafika wengi kwenye mitandao ya kijamii, huku saini ya mtandaoni 'petition' aliyoianzisha kupata zaidi ya sahihi 36,000 za kuunga mkono suala hilo.

 

Walt Disney ambayo hutengeneza filamu za watoto, hutumia msemo wa 'Hakuna Matata' ambao asili yake ni nchi za Afrika Mashariki, kama nembo ya kibiashara ya filamu hiyo, ambayo pia inaelezea maisha ya familia ya Kifalme ya Simba anayepatikana barani Afrika, huku majina mengi ya wahusika wakitumia yenye asili ya Afrika.

Mpaka sasa kampuni hiyo haijajibu tuhuma hizo, iwapo itakubalki kuacha kuutumia ama la.