Thursday , 10th Aug , 2017

ZIkiwa zimebakia takribani siku tatu kuelekea katika Mkutano Mkuu wa Klabu ya Simba, baadhi ya wanachama wa timu hiyo chini ya Bodi ya Wadhamini wamefungua kesi kuzuia mkutano huo ambao unatarajiwa kufanyika mnamo Agosti 13 mwaka huu Jijini DSM.

Zuio la mkutano huo limewasilishwa leo na Wakili wa Bodi hiyo, Juma Nassor katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu chini ya hati ya dharula lengo likiwa kuomba Mahakama izuie mkutano huo kufanyika na kuwashtaki wananchama wanne ambao wanakaimu nafasi ndani ya klabu hiyo ambao ni Salim Abdallah, Iddy Kajuna na Dk.Arnold Kashembe.

"Tunaiomba Mahakama izuiwe mkutano huo kwa sababu ya maslahi ya haki, hivyo Mahakama itoe amri kwa kuwa Katiba ya Simba iliyosajiliwa na Rita mwaka 1975 na ndiyo imeunda Bodi ya Udhamini hadi hivi sasa haina rekodi yoyote inayoonyesha kwamba kuna mabadiliko ya mfumo mpya wa Katiba", amesema Wakili Nassoro.

Pamoja na hayo, Wakili Nasoro amesema wanaokaimu nafasi za viongozi wa klabu hiyo ambayo kwa sasa wapo rumande hawana mamlaka kutokana hawajakidhi vigezo kwa kuwa inatakiwa Makamu wa Rais wa Simba ndiyo aitishe.

Kwa upande mwingine, siku ya kesho Mahakama ya Hakimu Mkazi ya Kisutu inatarajiwa kusikiliza na kutoa uamuzi juu ya pingamizi hilo lililofunguliwa Mahakama hapo.