Saturday , 7th Dec , 2019

Msemaji wa klabu ya Simba Haji Manara, ametangaza kuwa endapo msanii wa BongoFleva Ali Kiba akishindwa kuimba kwenye harusi yake basi hata akifa asiende kumzika.

Haji Manara upande wa (kushoto) na msanii Alikiba upande wa (kulia).

Haji Manara alizungumza hayo kwenye hafla ya chakula cha usiku kati ya wasanii na waandishi wa habari iliyyofanyika katika moja ya hoteli iliyopoa Masaki jijini Dar Es Salaam.

Kupitia EATV & EA Radio Digital Haji Manara ameeleza mipango yake ya kuoa ifikapo mwaka 2020 na lazima msanii Ali Kiba aimbe, akikataa au asipokuja basi hata kwenye msiba wake asiende,

"Sina Mke kwa sasa labda mnitafutie, nitaoa mwakani sisemi ni lini maana mtaniroga, ila ndiyo itakuwa mara ya kwanza Ali Kiba na wasanii wengine wataimba kwenye jukwaa moja aidha watataka au hawataki" amesema Haji Manara 

Pia ameendelea kusema "Nataka wajue mimi ndiyo kaka yao, Ali Kiba na wasanii wengine wataimba wakati mimi nitakapooa, kama hawataki mimi na wao uhusiano basi,  kwa sababu wote ni wadogo zangu, wakikataa kuja au kuimba hata nikifa Leo wasije" 

Aidha amesema Ali Kiba ni mwanaye na ndugu yake tangu udogoni ambaye  amekuwa anamuona mikononi mwake.