Friday , 16th Oct , 2020

Kundi kongwe la Mashabiki wa timu ya Simba Sc, la “Ngurumo za Simba” linalojumuisha mashabiki wa timu hiyo kutoka matawi na maeneo tofauti, wamefanya sherehe ya kutimiza miaka mitano tangu kuanzishwa kwa kundi hilo, kwa kufanya utalii wa ndani wilayani Bagamoyo mkoani Pwani.

Wakiongozwa na Mwenyekiti wa Kundi hilo Aboubakar Shaaban ambaye anahitimisha kipindi chake cha miaka minne ya Uongozi, amesema lengo la mashabiki hao licha ya kutoa sapoti kwa timu yao lakini pia ni katika kusaidiana katika mambo mbalimbali lakini pia hata kusaidia jamii kwa watu wenye uhitaji.

Kutoka kushoto ni Mwenyekiti wa Ngurumo za Simba Aboubakar Shaaban, Chriss Kabalika, Rais wa Mashabiki Goza Chuma na  Halima Ibadi.

Mwenyekiti Shaaban amesema kwa miaka kadhaa wamekuwa wakifanya sherehe zao Jijini Dar es Salaam, katika kumbi mbalimbali lakini safari hii wameamua kuipeleka wilayani Bagamoyo, ikiwa pia ni katika juhudi za kuhamasisha utalii wa ndani kwa wanamichezo nchini.

Katika Sherehe yao hiyo ya miaka mitano pia walimualika muendeshaji wa kipindi namba moja cha Mashabiki Afrika Mashariki kutoka East Africa Radio, cha Kipenga Xtra, Goza Chuma, maarufu kama “Rais wa Mashabiki” ikiwa ni heshima kwa  mchango wake kwa mashabiki wa timu mbalimbali nchini kwa kuwapa nafasi ya kuziongelea timu zao pamoja na mambo mbalimbali yanayofanywa na mashabiki mbali na kuzishangilia timu zao.