
Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Mwingulu Nchemba
Dkt. Nchemba alitoa maagizo hayo Jijini Dodoma alipokutana na wakuu wa Idara na Taasisi za wizara hiyo, katika kikao kazi kilicholenga kutekeleza maelekezo yaliyotolewa hivi karibuni na Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan, ambapo aliiagiza Wizara hiyo kutatua changamoto za wafanyabiashara nchini kuhusu masuala ya kodi.
“TRA nawataka mpeleke ujumbe makini kwa wafanyakazi wa TRA nchi nzima kwamba Serikali haijasema msikusanye kodi au mpunguze jitihada za kukusanya kodi hizo bali kinachoongelewa na kusisitizwa ni kukadiria na kukusanya kodi kwa kuzingatia sheria na taratibu, bila kuonea watu” - Dkt. Nchemba
Aidha Dkt. Mwigulu aliongeza kuwa “Mheshimiwa Rais alielezea changamoto ya Kushika akaunti, fedha za wafanyabashara, tuache vitendo hivyo, hapa hakuna mjadala ni lazima yafuatwe na sisi Wizara tutaendelea kufuatilia maelekezo hayo”.
Kwa upande mwingine Waziri huyo mpya wa Fedha akasisitiza, “Maelekezo ya Mheshimiwa Rais ni muhimu yatekelezwe ipasavyo ili kulinda na kukuza uchumi wa nchi kwa kutoza kodi kwa staha, weledi na kwa mujibu wa Sheria na turekebishe mahali tulipoharibu”.