Monday , 26th Apr , 2021

Makamu wa Rais wa wa Tanzania Dk. Philip Mpango amesema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar, imefanikiwa kutatua changamoto kumi na tano za Muungano kati ya changamoto ishirini na tano, huku wakiendelea na jitihada za kutatua zilizobaki.

Makamu wa Rais wa wa Tanzania Dk. Philip Mpango

Dk. Mpango amesema hayo wakati akifungua Kongamano la kuadhimisha miaka 57 ya Muungano wa Tanganayika na Zanzibar, Jijini Dodoma, na kusema kuwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ni tunu na urithi mkubwa kwa taifa letu na hatuna budi kuulinda, kuutunza na kuendelea kuelimisha umma kuhusu umuhimu wake.

"Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zanzibar zimefanikiwa kutatua changamoto 15 zilizokuwa zinaukabili muungano wetu kati ya changamoto 25, na jitihada zinaendelea kufanyika ili kuzipatia ufumbuzi changamoto zilizobakia" amesema Dk. Mpango

Aidha kufuatia kutokuwepo kwa sherehe za Muungano mwaka huu, Dk.Mpango amesema kwa mujibu wa Rais wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, fedha ambazo zilizokuwa zitumike kwa ajili ya sherehe hiyo zitagawanywa kwenda pande zote mbili za muungano. 

"Baada ya nchi yetu kuondokewa na mmoja wa mashujaa wake Hayati Dk John Magufuli tuliamua badala ya sherehe, tuadhimishe muungano wetu adhimu kwa kuwa na kongamano hili, kwa busara za mama yetu Mhe. Samia Suluhu ameagiza fedha ambazo zilizokuwa zitumike kwa ajili ya sherehe mwaka huu zitagawanywa kwenda pande zote mbili za muungano, na zitaamua namna ya kutumia fedha hizo kwa ajili ya shughuli za maendeleo"- amesema Dk. Mpango

Awali Dk. Mpango akianza kuhutubia umma uliopo kwenye kongamano hilo amemshukuru Mungu kwa kuliepusha taifa na Kimbunga JOBO ambacho kwa mujibu wa taarifa kutoka kwenye Mamlaka za Hali ya hewa kilitajariwa kutuwa katika kanda ya pwani jana tarehe 25/04/2021.

"Napenda kumshukuru Mungu na balaa kubwa lililokuwa huko baharini, sasa tuko salama hilo jamaa lililokuwa limetanda huko hili lituharibie nyumba limepotea kabisa"- amesema Dk. Mpango