Saturday , 24th Jul , 2021

Kocha wa Manchester United Ole Gunnar Solskjaer amesaini Mkataba wa miaka mitatu wa kuendelea kukinoa kikosi hicho cha mashetani wekundu mpaka mwaka 2024, mkataba huo ukiwa na kipengele cha kuongeza mwaka mmoja zaidi.

Ole Gunnar Solskjaer

Solskjear alitangazwa kuwa kocha wa muda wa Manchester United Disemba 2018 akichukua nafasi ya kocha Jose Mourinho kabla ya mwezi Machi 2019 kutangazwa rasmi kuwa kocha mpya wa kikosi hicho kwa mkataba wa miaka mitatau (3) mkataba ambao ulikuwa unamalizika mwishoni mwa msimu wa 2021-22.

Baada ya kusaini mkataba mpya kocha huyo raia wa Norway amesema

“Kila mtu anajua hisia zangu kwa klabu hii, na ninafurahi kusaini mkataba mpya. Ni wakati wa furaha kwa Manchester United, tumeunda kikosi kilicho na usawa mzuri wa vijana na wachezaji wazoefu ambao wana njaa ya mafanikio”.

Ole Gunnar bado hajashinda kombe hata moja akiwa na kikosi hicho na amekiongoza kwenye michezo 151 kwenye mashindano yote aameshinda michezo 86, sare michezo 34 huku michezo aliyopoteza ni 33, wastani wake wa ushindi ni asilimia 55.63.