Friday , 21st Oct , 2022

Waziri wa Habari Nape Nnauye, amewataka wasichana nchini kutumia uwepo wa TEHAMA katika kutatua changamoto zilizopo kwenye sekta mbalimbali zinazohusu jamii nchini ikiwemo sekta ya kilimo ambayo ina watu zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania.

Waziri wa Habari Nape Nnauye

Waziri Nape ametoa kauli hiyo leo Oktoba 21, 2022, jijini Dar es Salaam wakati alipokutana na wasichana kutoka taasisi ya Apps and Girl ambao walishiriki mashindo ya ugunduzi na teknolojia yaliyofanyika nchini Uswisi mwezi  wa 10 mwaka huu na kushika nafasi ya pili.

Ambapo amesema bado kundi la wasichana lipo chini katika ushiriki wa TEHAMA hivyo ni vyema wanafunzi wa kike wakaongeza kasi katika kusoma masomo ya sayansi ili kupata wataalamu watakaotumia fursa za teknolojia zilizopo katika sekta mbalimbali ikiwemo sekta ya kilimo..

Kwa upande wake Waziri wa Kilimo Hussein Bashe, amesema sekta ya kilimo ina uhitaji mkubwa wa teknolojia ili kufanikisha adhma ya kutengeneza kilimo cha kisasa kitakacho vuta vijana wengi kuingia katika uzalishaji kupitia kilimo cha mazao.

Kwa upande wake Slvia Balwire kutoka kampuni ya simu za mkono ya Tigo ambao wamewawezesha vijana hao kushiriki  pamoja na baadhi ya washiriki wa mashindano hayo amesema lengo la kuwakusanya wasichana hao kupitia Apps and Girls na kushiriki mashindano ya ubunifu ni kuongeza idadi ya wahandisi wa teknolojia wanawake ili kupata wataalamu wa sayansi na teknolojia wenye sifa na kushindana na mabadiliko ya teknolojia.