Thursday , 2nd May , 2024

Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) nchini imesema kwamba mgandamizo mdogo wa hewa katika Bahari ya Hindi mashariki mwa pwani ya Mtwara umeendelea kuimarika na kuwa kimbunga "HIDAYA" chenye nguvu ya kati, kikiwa umbali wa takribani kilomita 506 mashariki mwa pwani ya Mtwara

TMA imesema mwenendo wa mifumo ya hali ya hewa baharini inaonesha uwezekano mkubwa wa kimbunga Hidaya kusogea karibu kabisa na pwani ya Tanzania kuanzia usiku wa leo tarehe 02 Mei 2024 na kuendelea kuwepo hadi tarehe 06 na kwamba kimbunga hicho kinatarajiwa kupungua nguvu baada ya tarehe 6 Mei 2024.

"Uwepo wa kimbunga "HIDAYA" karibu na pwani ya nchi yetu unatarajiwa kutawala na kuathiri mifumo ya hali ya hewa hapa nchini ikiwa ni pamoja na kusababisha vipindi vya mvua kubwa na upepo mkali katika baadhi ya maeneo ya mikoa ya Mtwara, Lindi, Pwani (ikijumuisha visiwa vya Mafia), Dar es Salaam, Tanga, Morogoro, visiwa vya Unguja na Pemba na maeneo ya jirani hususan tarehe 3 Mei 2024 kwa maeneo ya pwani ya kusini (Lindi na Mtwara) na kusambaa katika maeneo mengine ya ukanda wa pwani kuelekea tarehe 4 hadi 6 Mei 2024," imeeleza taarifa ya TMA