Alhamisi , 2nd Jul , 2020

Gari nne yakiwemo malori mawili ya mafuta yamegongana na kusababisha ajali katika eneo la Mlandizi mkoani Pwani usiku wa kuamkia leo Julai 2.

Ajali ya Pwani

Ajali hiyo imetokea majira ya saa 5 Usiku wa jana Julai Mosi, na kupelekea kifo cha mtu mmoja na majeruhi watatu ambao wote wamekimbizwa katika Hospitali ya Tumbi.

Akithibitisha taarifa hiyo, Kamanda wa Polisi mkoani Pwani, Wankyo Nyigesa amemtaja marehemu kwa jina la Rahim Kurwa, huku akisisitiza kuwa abiria wanaotokea Dar es Salaam kwa kutumia barabara ya Morogoro watumie barabara ya Bagamoyo.

"Majeruhi wapo katika hospitali ya Tumbi pamoja na mwili wa marehemu lakini ninawashauri wasafiri wanaotokea Dar es Salaam watumie barabara ya Bagamoyo ili tuweze kuifungua hii barabara kwa sababu foleni ni kubwa sana", Kamanda Nyigesa.