Alhamisi , 18th Apr , 2019

Mtendaji Mkuu wa Temesa, Mhandisi Japhet Masele amesema kwamba mpaka sasa tayari kivuko cha Mv.Nyerere kimesharekebishwa injini zote na zinafanya kazi.

Picha ya kivuko cha Mv Nyerere

Akizungumza na East Africa Drive ya East Africa Radio, Mhandisi Masele amesema kwamba Kivuko cha Mv Nyerere kilipata matatizo kwenye mitambo yake kwa kuwa kiliangukia ndani ya maji.

Amesema mitambo hiyo ya kielektroniki ikiingia maji ndiyo huleta matatizo lakini, uharibifu kwenye kivuko hicho siyo mkubwa sana hivyo katika mwaka huu wa fedha, ifikapo Julai matengenezo ndiyo yataanza kufanyika.

"Kivuko kiliangukia kwenye maji na siyo kwenye sehemu ngumu kwa hiyo uharibifu siyo mkubwa sana. Uharibifu upo kwenye mitambo ya kuendeshea ambayo ikiingia maji inaathirika" amesema.

Pamoja na hayo, Mhandisi Masele amesema kwamba hadi sasa hawajafahamu matengenezo ya kivuko hicho yatagharimu shilingi ngapi kwa kuwa bado wanaendelea na manunuzi ya vifaa.

Kivuko cha MV Nyerere kilichokuwa kinafanya safari zake kati ya Bugorara na kisiwa cha Ukara katika Ziwa Victoria kilizama na kumpelekea idadi ya watu 200 wakiripotiwa kufariki.