Ijumaa , 12th Jan , 2018

Jeshi la Polisi mkoani Mwanza linawashikilia watu sita akiwemo Afisa ardhi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilemela, Aloyce Nyabange na mchora ramani wa viwanja Dedatus Mbeti kwa tuhuma za utapeli wa kuuza viwanja feki na kughushi nyaraka,

mbalimbali za serikali na kujipatia fedha kwa udanganyifu.

Akizungumza na waandishi wa habari, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Naibu Kamishna, Ahmed msangi amewataja watuhumiwa wengine kuwa ni Alex Josehat mkazi wa Buswelu mfanyabiashara, Juma Malulu Mkulima, Getruda Buberwa ambaye ni Sekretari kwenye ofisi ya Nyambari Nyegezi na Evansi Wilson mkazi wa Buzuruga.

Aidha Kamanda Msangi amesema taarifa hizo wamezipata baada ya watuhumiwa hao kumtapeli Barnabas Nibego ambaye alitoa taarifa kwa jeshi la polisi  kuhusu kutapeliwa na watu hao baada ya kubaini kauziwa kiwanja feki.

Kamanda Msangi amesema ushahidi utakapokamilika watuhumiwa hao wataishwa mahakamani.

Mbali na watu hao kuuza viwanja feki wanatuhumiwa pia kughushi taarifa za benki vitambulisho vya kupigia kura pamoja vyeti vya ngazi mbalimbali za elimu.