Jumatatu , 23rd Mei , 2016

Mbunge wa Jimbo la Temeke Abdallah Mtolea CUF ameliambia Bunge leo Mjini Dodoma kwamba bei ya sukari kupanda na kuadimika kumesababisha mama ntilie katika jimbo lake kufilisika kwa kuuza chai na vyakula kwa bei ileile pamoja na kupanda bei ya sukari.

Mtolea ameyasema hayo wakati akiuliza swali la nyongeza katika wizara ya viwanda na biashara akitaka kujua kwa nini serikali isiwe na utaratibu wa kutoa ripoti kila siku kuhusu upatikanaji wa sukari nchini.

Akijibu swali hilo Waziri wa Viwanda na Biashara Charles Mwijage amesema kwamba mama ntuilie ni watumishi wa Mungu na serikali inawapongeza kwa kuendelea kuwahudumia wananchi kipindi hiki ambapo serikali inaendelea na juhudi zake za kutaka kumaliza tatizo la sukari nchini.

Kuhusu serikali kutoa ripoti ya upatikanaji wa sukari nchini Waziri amesema atafanya hivyo kuanzia kikao cha leo mchana ili wananchi waweze kupata undani na uhakika wa hali ya sukari kwa wakati husika.