Jumatatu , 20th Mei , 2019

Shirikisho la Soka Tanzania TFF limetangaza orodha ya waamuzi watakaochezesha mchezo wa kirafiki wa Kimataifa kati ya Simba na Sevilla ya Hispania.

Wachezaji wa Simba na Sevilla

Timu hizo zinatarajia kucheza mchezo wa kirafiki wa Kimataifa kwa udhamini wa kampuni ya SportPesa, Mei 23 katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam, majira ya saa 1:00 usiku.

Kupitia ukurasa wa Twitter, TFF imewataja waamuzi hao, wote wakiwa ni wa kutoka hapa nchini.

Kabla ya mchezo huo, Mei 21, Simba itacheza na Singida United katika uwanja wa Namfua, huku Simba ikihitaji pointi moja pekee ili iweze kutangaza ubingwa wao wa pili mfululizo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.

Pia taarifa iliyotolewa kupitia tovuti ya klabu ya Sevilla, inaeleza kuwa klabu hiyo itawasili nchini Jumanne, Mei 21 na kikosi kamili kilichocheza mchezo wa mwisho wa LaLiga wikiendi iliyopita dhidi ya Athletic Club Bilbao.