
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Azam Fc, Zacharia Thabit akiwa katika studio za East Africa Radio.
Zaka Zakazi ameyasema hayo baada ya Azam kufungwa na Mtibwa Sugar kwa bao 1-0 na kuhitimisha mwendo wao wa kushinda mechi 7 mfululizo kulikowafanya wakamate usukani wa ligi wakiwa na alama 21 .
''Mchezo ulikua mgumu sana, Mtibwa walicheza wakipigania mambo mawili kwanza kuifunga timu iliyokua haijafungwa na pia kupata alama tatu muhimu,.
Kufungwa si jambo zuri, lakini mkifungwa kuna jambo zuri la kujifunza, kabla ya mchezo niliongea na wachezaji akiwemo Frank Domayo, alikiri kuwa na presha kubwa ya kuendeleza kutunza rekodi, jambo ambalo naamini tusingefungwa tusingetulia, kufungwa ni kengere ya tahadhali kwetu ili tujipange kwa ajili ya mechi zijazo.
Mkuu huyo wa Idara ya Habari na Mawasiliano wa Azam Fc ameongeza kwamba walishaionesha Tanzania kwamba wanauwezo wa kushinda, lakini moja ya sifa ya timu yoyote ni pamoja na kufungwa.
Azam inasalia kileleni mwa msimamo wa VPL wakiwa na alama 21 katika michezo 8, wakiwa juu ya Yanga ambayo imesalia kuwa ndio timu pekee ambayo haijafungwa katika ligi kuu wakiwa nafasi ya pili kwa alama zao 17 katika mechi 7.