Ijumaa , 14th Oct , 2016

Katibu Mkuu Mteule wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema kipaumbele chake cha kwanza ni kushughulikia ukosefu wa amani duniani ambao amesema ndiyo changamoto kubwa hivi sasa.

Amesema hayo wakati akizungumza kwa mara ya kwanza kabisa katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani baada ya kupitishwa na Baraza Kuu.

Bwana Guterres, amesema mizozo ya zamani imeendelea kuwepo, mipya ikiibuka huku ukwepaji sheria ukizidi kushamiri hivyo na kusema kuwa ongezeko la matumizi ya diplomasia katika kusaka amani itakuwa kipaumbele changu.

Aidha Bw. Guterres amesema kuna changamoto kubwa kuhusiana na marekebisho ya chombo hiki kiweze kuwa na ufanisi na uwezo wa kutekeleza majukumu yake kwa watu tunaowahudumia ulimwenguni kote.