Ijumaa , 26th Mar , 2021

Mkuu wa Majeshi Jenerali Venance Mabeyo, amemuomba Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. Samia Suluhu Hassan, kukutana naye ofisini kwake ili aweze kumuambia dokezo alilodokezwa na aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Dkt. John Magufuli.

Mkuu wa Majeshi, Jenerali Venance Mabeyo

Jenerali Mabeyo ametoa kauli hiyo hii leo Machi 26, 2021, Chato mkoani Geita, wakati wa ibada maalum ya mazishi ya Hayati Dkt. John Magufuli, ambaye atazikwa leo alasiri katika makaburi ya familia yaliyopo nyumbani kwake Chato.

"Mheshimiwa Rais (Samia) binafsi Hayati Dkt. Magufuli alinidokeza, lakini ninaomba nisilitoe dokezo hilo hapa nitakuomba nikuone ofisini, " ameeleza Jenerali Venance Mabeyo.

Aidha, Jenerali Mabeyo, amempongeza Rais Samia, na kumuahidi kuwa watahakikisha vyombo vya ulinzi na usalama vinamlinda, "Vyombo vya ulinzi na usalama vinapenda kukuhakikishia kuwa ulinzi wa nchi na mipaka yake ni salama na kwamba vitaendelea kukulinda wewe, kukutii na kutekeleza majukumu yake aidha vinakuhakikishia utiifu, uadilifu na uaminifu mkubwa kwako kama ilivyo mila na desturi ya majeshi yetu".