Thursday , 6th Oct , 2016

Wakurugenzi wa halmashauri na wale wa hospitali za umma nchini wamepewa siku sitini kuanzia jana wawe wamewalipa posho za wauguzi za kununua sare za kazi ya shilingi laki moja na elfu ishirini pamoja na malimbikizo ya posho hizo.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu, akiongea na wauguzi (hawapo pichani) wakati wa ufunguzi wa mkutano wa 44 wa wauguzi Tanzania

Agizo hilo limetolewa mkoani Kigoma na Waziri wa Afya,Maendeleo ya Jamii,Jinsia ,Wazee na Watoto Ummy Mwalimu wakati wa ufunguzi wa mkutano mkuu wa 44 wa wauguzi Tanzania.

Waziri Ummy amesema asilimia themanini ya kazi zote kwenye sekta ya afya nchini zinafanywa na wauguzi, hivyo kuwataka wakurugenzi kuzingatia miongozo iliyopo ya Serikali,

“Kama mwongozo ni kulipa elfu thelathini lipa thelathini si vinginevyo. Serikali imekwishatoa waraka wa kazi za ziada yaani “extra duty circular” ambao unapaswa kufuatwa hata mnapofanya kazi usiku kwani kuna masaa ya ziada”.

“Nawaagiza waajiri wote kuzingatia nyaraka hizi ili kuondoa malalamiko yasiyo ya lazima, Hili ni suala muhimu kwani mnakuwa kazini siku tano hadi sita kwa wiki hivyo mnahitaji sare walau tano ili muweze kubadilisha kila mara. Serikali itatoa waraka wa si chini ya laki tatu kulingana na hali ya uchumi itavyokuwa. Natumaini waraka huu utatoka mapema na kuanza kutumika mwaka ujao wa fedha hivyo kwa mwaka huu tuendelee kutumia waraka uliopo.

Aidha, aliagiza baada ya siku sitini alizotoa kupatiwa orodha za halmashauri ambazo hazitokuwa zimewalipa posho hizo na mikoa ipi”kwani kuna wauguzi wangapi hadi mshindwe kuwapa posho za sare ,mnataka wauguzi hawa waje kazini wawe wamevaa nini?aliuliza Waziri.

Kuhusu upungufu mkubwa wa wauguzi Waziri Ummy alisema ni kweli kuwa, nchi inakabiliwa na changamoto kubwa ya uhaba wa wauguzi hali inayopelekea muuguzi mmoja kuhudumia wagonjwa wengi zaidi ya uwezo wake, mazingira hayo yanaweza kuathiri ubora wa huduma wanayotoa.

Wauguzi nchini wamekuwa na utaratibu wa kukutana kitaifa na kuelimishana juu ya maadili, majukumu ya viongozi wa chama katika utoaji wa huduma za afya kwa weledi kwa magonjwa ya kuambukiza na yasiyo ya kuambukiza.

Mkutano huo umebeba ujumbe maalumu na kauli mbiu ya mwaka huu ni “Wauguzi: Nguvu ya mabadiliko, uboreshaji wa uthabiti wa mfumo wa afya.

Wauguzi toka mikoa mbalimbali nchini wakimsikiliza waziri wa afya wakati wa mkutano huo,ambapo kwenye hotuba yao waliomba kulipwa posho na malimbikizo ya sare za wauguzi kiasi cha shilingi 120,000/=
Wakati watanzania wakiendelea kuchanga fedha na mahitaji mengine kwa waathirika wa tetemeko la ardhi lililotokea mkoani Kagera, Wauguzi waliohudhuria mkutano huo nao walichanga kiasi cha shilingi 4,196,500/= na kumkabidhi Waziri Ummy Mwalimu ili afikishe mchango wao na pole kwa mkoa huo