Wednesday , 20th Dec , 2017

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Binilith Mahenge amesema Mji wa Dodoma hauna sababu ya kuwa mchafu tena baada ya kukamilika kwa ujenzi wa dampo la kisasa lenye uwezo wa kuhudumu kwa miaka mingi.

Dkt. Mahenge ameyasema hayo baada ya kutembelea dampo hilo ambalo limejengwa na Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma, katika eneo la Chidaya Kata ya Matumbulu nje kidogo ya Dodoma mjini.

Mhandisi wa Mazingira wa Manispaa ya Dodoma Barnabas Faida, amesema dampo hilo linatumia teknolojia ya kuzika taka ardhini (Sanitary Landfill) ambayo ni rafiki kwa mazingira na afya za wakazi wa maeneo ya karibu na dampo.

Dampo hilo ambalo tayari limeanza kufanya kazi limejengwa kwa fedha za mradi wa kuimarisha Miji ya Kimkakati Tanzania (TSCP) unaofadhiliwa na Benki ya Dunia na kuratibiwa na Ofisi ya Rais-TAMISEMI.