Friday , 13th Dec , 2019

Mama Mzazi wa Mwandishi wa Habari, Erick Kabendera, anayekabiliwa na mashtaka ya uhujumu uchumi, amemuangukia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt John Pombe Magufuli, na kumuomba amsamehe mwanaye ili arudi nyumbani na kuendelea kumlea.

Mama wa Mwandishi wa Habari, Erick Kabendera, Verediana Mjwahuzi

Mama Erick Kabendera, anayejulikana kwa jina la Verediana Mjwahuzi, ametoa ombi hilo leo Disemba 13, 2019, na kusema kuwa Erick ndiye mtoto pekee aliyekuwa akimsaidia katika huduma zake za matibabu na kuomba kuwa kama ambavyo Rais Magufuli analea wazazi wake, basi na yeye aangaliae namna ya kumuachia mwanaye.

"Mungu alimzawadia Erick kusudi mimi anitunze na yeye ni mtoto kwa wazazi pamoja na kuwa ni mkubwa lakini cheo chake cha Urais hakimzuii kuwa mtoto wa mtu ana wazazi na anawalea kwahiyo namuomba sana anifikirie, anione nilivyo, nahangaika, maisha yamekuwa magumu, magonjwa dawa sizipati, amruhusu huyu mwanangu na mimi anitunze kama na yeye anavyotunza wazazi wake, watu wanasema mengi dhidi ya mwanangu, naomba hayo wanayomuambia achambue" amesema Mama Erick Kabendera.

Kabendera anakabiliwa na mashtaka matatu, likiwemo la uhujumu uchumi, ukwepaji wa kodi pamoja na kuongoza genge la uhalifu, makosa ambayo anadaiwa kuyatenda kati ya Januari 2015 na Julai 2019, maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam.