Alhamisi , 6th Jan , 2022

Kuelekea mashindano ya AFCON yanayotarajiwa kuanza kutimua vumbi kuanzia Januari 9, Kocha mkuu wa timu ya Taifa ya Sierra Leone, John Keister ameweka wazi kuwa amepokea vitisho vya kuuawa kabla ya kutangaza kikosi cha cha taifa hilo kwa ajili ya michuano kombe la Mataifa ya Afrika.

Kocha mkuu wa timu ya Taifa ya Sierra Leone, John Keister (Kulia) akikabidhiwa jezi baada ya kutambulishwa.

Kocha huyo mwenye umri wa miaka 51 amepokea vitisho mara mbili kuhusu kujumuishwa kwa wachezaji fulani ambao hawajatajwa ikiwa ni siku moja kabla ya kutangaza kikosi cha wachezaji 28 watakaoshiriki michuano ya AFCON nchini Cameroon.

Hata hivyo Kocha huyo ameshatoa taarifa kwenye mamlaka za ulinzi nchini Sierra Leone ambapo uchunguzi bado unafanyika kubaini wanaohusika na vitisho hivyo.

Keister amesema kuwa anasikitishwa na kitendo hicho, akitanabaisha kuwa isingefikia kwenye hatua hiyo na kuacha kikosi hicho kucheza michezo yake na baadaye kumuhukumu kutokana na matokeo ikizingatiwa  ni kwa mara ya kwanza wanashiriki kwenye AFCON tangu 1996.