Wednesday , 3rd Aug , 2022

Msimu mpya wa Ligi kuu soka Tanzania bara NBC Premier League 2022-23 utaanza kutimua vumbi rasmi Agosti 15, 2022. Na Ligi itamalizika Mei 27, 2023. Ligi ina jumla ya timu 16 na itachezwa jumla ya michezo 240 kukamilisha msimu.

Mchezo wa raundi ya kwanza wa Simba na Yanga Dabi ya Kariakoo utachezwa Oktoba 23, 2022

Ligi itafunguliwa rasmi Agosti 13 kwa mchezo wa ngao ya Jamii ambao utazikutanisha timu za Kariakoo Simba na Yanga na siku mbili baadae rasmi Ligi itaanza. Michezo ya raundi ya kwanza itachezwa kwa siku 3 Agosti 15, 16 na 17.

Agosti 15 itachezwa michezo miwili timu ya Ihefu ya jijini Mbeya watakuwa wenyeji wa Ruvu Shooting ya Pwani, Namungo FC ya Lindi wataminyana na Mtibwa Sugar ya Morogoro. Agosti 16 itachezwa michezo 3, Singida big Stars  ya Singida watakuwa wenyeji wa Tanzania Prisons ya Jijini Mbeya, Polisi Tanzania ya Moshi Kilimanjaro watawakaribisha mabingwa watetezi wa Ligi Yanga SC na Dodoma jiji wataminyana na Mbeya City.

Raundi ya kwanza itakamilishwa Agosti 17 kwa michezo 3 ambapo Coastal Union ya Tanga watakuwa wenyejeji wa KMC FC ya Dar es salaam, Simba SC watawaarika Geita Gold FC ya mkoani Geita na Azam FC ya Dar es salaam watacheza dhidi ya Kagera Sugar ya Bukoba Kagera.

Mchezo wa raundi ya kwanza wa watani wa jadi Simba na Yanga Dabi ya Kariakoo utachezwa Oktoba 23, 2022 mchezo huu utachezwa uwanja wa Benjamini Mkapa Dar es salaam. Kwa mujibu wa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi TPLB Almas Kasongo amesema upangaji wa ratiba ya msimu huu umezingatia kalenda ya michuano ya kimataifa ya FIFA na CAF lakini pia michuano ya Mapinduzi Cup na Ligi itasimama kwa vipindi 17 tofauti kupisha kalenda za CAF na FIFA.