Wednesday , 12th Oct , 2022

Meneja wa Habari na Mawasiliano wa klabu, Ahmed Ally amesema licha ya kufanikiwa kupata ushindi mnono katika mchezo wa mkondo wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Premiero De Agosto lakini bado hatujafuzu hivyo tutapambana Jumapili kuhakikisha tunaingia hatua ya makundi.

Ahmed amesema msimu uliopita walifanikiwa kushinda ugenini dhidi ya Jwaneng Galaxy lakini walipokuja nyumbani wakapoteza na kutolewa mashindanoni kitu ambacho hatutapenda kijirudie katika historia yetu.

Ahmed ameongeza kuwa hatuhitaji kufuzu hatua ya makundi kwa kutegemea ushindi tuliopata nchini Angola badala yake tumejipanga kushinda ili kuwapa furaha zaidi mashabiki wetu Jumapili.

“Sisi tulishinda mechi ya kwanza ugenini lakini bado hatujafuzu. Mechi ya Jumapili katika Uwanja wa Benjamin Mkapa ndiyo utatupa tiketi ya kufuzu hatua ya makundi. Premiero De Agosto si timu mbaya tunapaswa kujipanga vilivyo.

“Tunataka kufuzu hatua ya makundi kwa kushinda nyumbani sio kutegemea ushindi tuliopata Angola wiki iliyopita. Tunataka kuwapa furaha mashabiki wetu ambao tunaamini watakuja kwa wingi uwanjani,” amesema Ahmed.

Simba inatafuta nafasi ya kuingia kwenye hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Barani Afrika huku kwenye mchezo wa mkondo wa kwanza dhidi ya Primiero de Agosto walichomoza na ushindi wa magoli 3-1 ugenini mjini Luanda nchini Angola.