Jumanne , 8th Jan , 2019

Rais wa Benki ya Dunia, Jim Yong Kim ametangaza kujiuzulu Februari Mosi, ikiwa ni miaka mitatu kabla ya muhula wake kumalizika mwaka 2022.

Rais wa Benki ya Dunia, Jim Yong Kim.

Kim ambaye anajiunga na kampuni binafsi inayoangazia uwekezaji katika mataifa yanayoendelea, amesema imekuwa ni heshima kubwa kwake kuiongoza taasisi hiyo muhimu.

Ofisa Mkuu wa Benki ya Dunia, Kristalina Georgieva, atachukua nafasi ya rais wa mpito baada ya Kim kuondoka. Kim alianza kipindi chake cha pili kama Rais wa Benki ya Dunia, Julai, 2017.

Alichukua mikoba ya Robert Zoellick mwaka 2012, chini ya rais wa zamani wa Marekani, Barack Obama.

Taasisi hiyo inayohusika na kufadhili miradi katika nchi zinazoendelea, kwa kawaida imekuwa ikiongozwa na raia wa Marekani.

Taasisi hiyo ilianzishwa mwishoni mwa Vita Kuu ya Pili ya Dunia sambamba na Shirika la Fedha Duniani, IMF ambalo huongozwa na raia wa Ulaya.