Jumatatu , 28th Aug , 2017

Rais mstaafu wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Kikwete amesema mimba haipaswi kuwa ugonjwa na juhudi zinatakiwa zichukuliwe katika kuhakikisha mama na mtoto hawapotezi uhai wakati wa kujifungua.

Dkt. Kikwete ameitoa kauli hiyo akiwa nchini India akiwa kwenye ziara iliyomfanya ajifunze namna ambayo taifa hilo limefanikiwa kupunguza vifo vya kinamama wajawazito.

"Mimba siyo ugonjwa,tufanye kila tuwezalo mama na mtoto wasipoteze uhai wakati wa kujifungua.Tukio la kujifungua lapaswa kuwa shangwe si huzuni kama ambavyo imekuwa mara nyingine kwenye familia tofauti", alisema Dkt. Kikwete.

Rais huyo mstaafu anafanya ziara yake nchini India yenye lengo la kujifunza ni kwa namna gani vifo vya kinamama wajawazito pamoja na watoto chini ya umri wa miaka mitano vimeweza kudhibitiwa nchini humo.