Jumamosi , 18th Jan , 2020

Rapa Mabeste amesema alikuwa anatamani kuwepo na amani kati yake na marehemu Pancho Latino kabla ya kufariki, jambo ambalo linamuuma na linamfanya kuaamini hata yeye na waliobakia wanaweza kuondoka duniani muda wowote.

Picha ya msanii Mabeste

Mabeste ameyazungumza hayo kupitia EATV & EA Radio Digital, baada ya kumaliza tofauti zake na Producer Hermy B siku kadhaa zilizopita ambaye ni kiongozi wa studio za B-hitz, mahali alipokuwa anafanyia kazi Pancho Latino.

"Kiubinadamu nilitamani kupatana naye kipindi kile tulichogombana mwaka 2013, nilitaka baada ya miezi mitatu hasira ziwe zimeisha kwa kila mmoja wetu, nilikuwa natamani tena ule uwepo wa kurudi kufanya kazi pamoja lakini ilishindikana kwa sababu kipindi kile marehemu Pancho alikuwa yupo hai" ameeleza Mabeste.

Aidha msanii huyo wa HipHop ameongeza kusema "Pancho aliingia kwenye ule ugomvi kwa sababu kama nagombana na bosi basi hata wafanyakazi wake hatuwezi kuwa sawa, mimi binafsi kutoka moyoni mwangu kilikuwa kinaniuma sana kwa sababu Pancho amefariki hatupo sawa, nilikuwa natamani kuwepo na amani kwa sisi tuliobakia".