Jumatatu , 24th Sep , 2018

Msanii wa muziki wa kizazi kipya bongo, Mo Music amefunguka na kujigamba kuwa yeye ni miongoni mwa watu waliowahi kutabiriwa katika ukoo wao na bibi yake mzaa baba yake mzazi, kuja kuwa msanii mkubwa wa muziki nchini licha ya kuwa alipotea kidogo kwenye 'game'.

Msanii wa muziki wa kizazi kipya bongo, Mo Music.

Mo Music ameeleza hayo alipokuwa anazungumza kwenye PLANET BONGO ya East Africa Radio muda mchache kabla ya kutambulisha kazi yake mpya ya 'umesahau' na kusema kuwa enzi za uhai wa bibi yake huyo alikuwa anapenda sana muziki na ndiye aliyemtabiria kipaji chake.

"Moja ya vitu ambavyo vilivyowahi kutabiriwa katika ukoo wetu ni kutokea mtu ambaye atakuwa mkubwa sana kwenye sanaa na inawezekana ikwa ni mimi, kwasababu kwenye ukoo wetu hakuna msanii mwingine zaidi yangu", amesema Mo Music.

Mbali na hilo, Mo Music amesema ameweza kutimiza malengo yake na kubadilisha baadhi ya vitu katika maisha yake kupitia muziki kwa zaidi ya asilimia 60 na kudai kwa sasa anajivuta zaidi ili aweze kukamilisha mengine.

Mo Music ni miongoni mwa wasani walioweza ku-hit kwenye miaka ya 2014 na kibao chake cha 'basi nenda' ambacho kilikuwa gumzo kila mahali hususan kwa watu waliokuwa wanaachana kwenye mahusiano yao wakikitumia kama ishara ya kuruhusu kuondoka au kuachilia jambo fulani.