Jumatatu , 15th Jun , 2020

Baada ya kusambaa kwa picha mitandaoni zikimuonesha msanii wa HipHop Wakazi, akipewa kadi ya uanachama na viongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, leo hii amejitokeza kueleza lengo lake la kujiunga na chama hicho.

Msanii Wakazi akiwa na kiongozi wa Chama Cha ACT-Wazalendo

Wakazi ameeleza hilo kupitia katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Instagram, ambapo ameandika ujumbe ambao unaeleza kuwa,

"Nikiwa kama mzalendo, mpenda maendeleo, mwanaharakati wa uwazi, haki na usawa, ninayo furaha kuutangazia umma wa Tanzania kuwa rasmi nimejiunga na umoja wa wanafamilia wa ACT Wazalendo kuanzia siku ya jana, tunaishi kwenye nchi ya kidemokrasia inayoruhusu vyama vingi na kila mtu ana uhuru wa kujiunga na chama anachokipenda na kinachoendana na itikadi na sera ambazo yeye binafsi anazoziamini" ameandika.

"Mimi Webiro "Wakazi" Wassira, ninadiriki kusema  nina imani na ACT Wazalendo, kama chama bora kabisa nchini ambacho kitalipeleka Taifa kwenye njia sahihi kabisa ya kuleta maendeleo ya kweli kwa watu wote, huku kikizingatia utawala na uongozi bora" ameongeza.