Alhamisi , 12th Dec , 2019

Msemaji wa klabu ya Simba, Haji Manara, amefunguka kuwa yeyote anayesema kuhusu kuonewa na kufukuzwa kwa aliyekuwa kocha wao Patrick Aussems, basi amfuate hukohuko alipoenda.

Msemaji wa Klabu ya Simba, Haji Manara.

Haji Manara amejibu hivyo kupitia EATV & EA Radio Digital, baada ya kuwepo na maoni mengi ya mashabiki wa klabu hiyo ya Simba, kusema kocha aliyefukuzwa ghafla hakustahili kufanyiwa hivyo.

"Kwa maana hiyo mnataka mseme Mohammed Dewji anayelipa pesa awe haipendi Simba na anamuonea, yaani pesa ziwe zake halafu awe anamuonea huyo mtu, yeye ndiyo mwenyekiti wa bodi utasemaje amtetee mtu ambaye hayupo, tuungeni mkono, twendeni kwenye mpira tuna mechi na Yanga  pia tuna mechi kwenye Kombe la FA" ameeleza Haji Manara.

Aidha Haji Manara ameendelea kusema "Tutakwenda kuchukua ubingwa wetu, mimi nitaondoka, Aussems kaondoka, wataondoka wengine na wengine ila Simba itabakia palepale na itaendelea kuwepo, kama uliipenda Simba kwa ajili ya Aussems mfuate Aussems".

Klabu ya Simba siku ya Disemba 11, 2019, ilimtambulisha kocha wao mpya aitwaye Sven Vanderbroeck, raia wa Ubelgiji, na kocha msaidizi aliyetambulishwa ni mzawa Selemani Matola.