Jumamosi , 3rd Apr , 2021

Klabu ya Simba SC imefanikiwa kufuzu hatuaya robo fainali ya ligi ya mabingwa barani Afrika, baada kuibuka na ushindi wa mabao 4-1 dhidi ya klabu ya AS Vital ya Kongo, lakini pia mabingwa hao wa Tanznaia wamejihakikishia nafasi ya kumaliza vinara wa kundi A baada ya kufikisha alama 13.

Wachezaji wa Simba wakishangilia baada ya kufunga bao

Mabao ya Simba katika mchezo huo yamefungwa na Luis Miquissone dakika ya 30, Clatous Chama amefunga mara mbili dakika ya 45 na 84 na bao nyingine limefungwa na Larry Bwalya wakati lile la AS Vital limefungwa na Zemanga Soze dakika ya 32.

 

Ushindi huu unaifanya Simba ifikishe alama 13 na kuendelea kuongoza kundi wakiwa wanaongoza kwa tofauti ya alama 5 dhidi ya Al Ahly wenye alama 8 walio nafasi ya pili huku ukiwa umebakia mchezo mmoja kabla ya kumaliza michezo ya hatua ya makundi. Hivyo kwa ushindi wa hii leo Simba wamejihakikisha nafasi ya kumaliza nafasi ya kwanza kwenye msimamo wa kundi A.

 

Na baada ya mchezo mwingine wa kundi hilo kumalizika kwa sare ya bao 2-2 kati ya Al Ahly na AL Merreikh, kwa msimamo ulivyo sasa ni rasmi Simba na Al Ahly ndio zimefuzu hatua ya robo fainali kutoka kundi A, Simba wana alama 13 nafasi ya kwanza nafasi ya pili Al Ahly alama 8 nafasi ya tatu ni AS Vita wakiwa na alama 4 na Al Merreikh wana alama 2 na ndio wanaburuza mkia.