Jumatatu , 3rd Dec , 2018

Wakati klabu ya Yanga ikiwa Jijini Mbeya tayari kwa mchezo wa ligi kuu Tanzania bara dhidi ya Tanzania Prisons leo, imeendelea kuwakosa wachezaji wake kadhaa akiwemo nahodha Kevin Yondani.

Kikosi cha Yanga

Yondani hajaichezea klabu yake ya Yanga tangu aliporejea kutoka katika kambi ya timu ya taifa 'Taifa Stars' mwezi uliopita, ambapo taarifa mbalimbali zinadai kuwa mchezaji huyo anadai stahiki zake, jambo ambalo klabu imelipinga.

Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili wa klabu hiyo, Hussein Nyika, amefananua kuwa Yondani amebaki Jijini Dar es Salaam kumaliza matatizo yake binafsi ambayo yanamkabili hivyo hatocheza mechi ya leo.

Nyika amesema beki huyo mkongwe si kweli kuwa anaidai klabu bali ni mambo mengine yaliyosababisha ashindwe kusafiri na kikosi kuelekea Mbeya kwa ajili ya kipute hicho cha ligi.

"Ni kweli Yondani hajasafiri na timu, yupo Dar es Salaam kutokana na baadhi ya matatizo yanayomkabili na kuhusu kuidai Yanga si la kweli, ni mambo mengine tu yamesababisha asisafiri na timu," amesema.

Hivi karibuni Yondani aliwahi kukaririwa akisema kuwa ni kweli anaidai klabu yake lakini hiyo si sababu ya yeye kutoonekana uwanjani, akisisitiza kuwa atarudi kuitumikia klabu yake mambo yakikaa sawa.