Waziri wa Maliasili na Utalii Mohamed Mchengerwa, akiwa na Naibu waziri Mary masanja na Katibu Mkuu wake Dkt. Hassan Abbas
Wakichangia hoja zao kwenye semina maalum ya uhifadhi iliyoratibiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii leo Mei 29,2023 wabunge hao wamefafanua kuwa katika kipindi kifupi kumekuwa na maboresho makubwa katika uhifadhi wa raslimali ambapo wameomba juhudi zaidi zifanywe ili sekta hizo ziweze kutoa mchango zaidi katika uchumi wa taifa.
Akizungumza Mbunge Esther Matiko amempongeza Waziri wa Maliasili na Utalii, Mohamed Mchengerwa kwa kuweza kushughulikia mgogoro wa mipaka baina ya hifadhi ya Serengeti na vijiji vinavyoizunguka hifadhi hiyo kwenye wilaya ya Tarime ambapo amesema njia aliyoitumia ya ushirikishwaji ndiyo njia pekee inayoleta matokea chanya.
Akichangia katika semina hiyo, Mbunge Charles Mwijage ameiomba Wizara kuzingatia sheria na kuondoa mifugo yote ambayo imevamia maeneo mbalimbali ya hifadhi ambapo Mhe. Mchengerwa ametoa siku 14 kuondoa mifugo yote.
Mbunge wa Manyoni Mashariki, Mhe. Pius Chanya ameishauri serikali kuweka mikakati kabambe ya kutangaza vivutio mbalimbali vya utalii ikiwa ni pamoja na kufanya marekebisho makubwa katika mfumo wa taasisi zinazoshughulikia sekta ya utalii kwa kubadili Bodi ya Utalii kuwa Mamlaka.
Awali akizungumza katika semina hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Mohamed Mchengerwa amesema migogoro mingi inayojitokeza sasa kwenye maeneo ya hifadhi ni siyo ya maliasili na utalii bali imezalishwa na migongano ya sheria ambapo ammewasihi wabunge kuangalia namna bora ya kutunga sheria zinazokinzana.
Aidha, amesema rasilimali za misitu na nyuki huchangia asilimia 3.3 ya pato la Taifa, asilimia 5.9 ya mapato yatokanayo na biashara ya nje, na ajira takribani milioni 3 za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja.
Pamoja na faida hizo, hifadhi za wanyamapori na misitu ni muhimu kwa mifumo ikolojia ikiwa ni pamoja na uhifadhi wa bioanuai, kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, hewa safi na kuhifadhi vyanzo vya maji.
Ameongeza kuwa Sekta hizi zinakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo, ujangili, uvunaji haramu wa mazao ya misitu, uchimbaji haramu wa madini, uvamizi wa maeneo ya hifadhi kwa ajili ya shughuli za kulisha mifugo, kilimo na makazi na mioto haramu.