Monday , 29th May , 2023

Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Tanzania wameipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii Kwa Kazi nzuri inayoifanya ya kuhifadhi raslimali kwa faida ya vizazi vya sasa na baadaye huku wakisisitiza ushirikishwaji wa jamii zinazozunguka maeneo ya hifadhi.

Waziri wa Maliasili na Utalii Mohamed Mchengerwa, akiwa na Naibu waziri Mary masanja na Katibu Mkuu wake Dkt. Hassan Abbas

Wakichangia hoja zao kwenye semina maalum ya uhifadhi iliyoratibiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii leo Mei 29,2023 wabunge hao wamefafanua kuwa katika kipindi  kifupi  kumekuwa  na maboresho makubwa katika uhifadhi wa raslimali ambapo wameomba juhudi zaidi zifanywe ili sekta hizo ziweze kutoa mchango zaidi katika  uchumi wa taifa.

Akizungumza Mbunge Esther Matiko amempongeza Waziri wa Maliasili na Utalii, Mohamed Mchengerwa  kwa kuweza kushughulikia mgogoro wa mipaka  baina ya  hifadhi ya Serengeti na  vijiji vinavyoizunguka hifadhi hiyo kwenye wilaya ya Tarime ambapo amesema njia aliyoitumia ya ushirikishwaji ndiyo njia pekee inayoleta matokea chanya.

Akichangia katika semina hiyo, Mbunge Charles Mwijage ameiomba Wizara kuzingatia sheria na kuondoa mifugo yote ambayo imevamia maeneo mbalimbali ya hifadhi ambapo Mhe. Mchengerwa ametoa siku 14 kuondoa mifugo yote.

Mbunge wa Manyoni Mashariki,  Mhe. Pius Chanya ameishauri serikali kuweka mikakati  kabambe ya kutangaza vivutio mbalimbali vya utalii ikiwa ni pamoja na kufanya marekebisho makubwa katika mfumo wa taasisi zinazoshughulikia sekta ya utalii kwa  kubadili Bodi ya Utalii kuwa Mamlaka.

Awali akizungumza katika semina hiyo, Waziri wa Maliasili na Utalii, Mohamed Mchengerwa amesema migogoro mingi inayojitokeza sasa kwenye maeneo ya hifadhi  ni  siyo ya maliasili na utalii bali imezalishwa  na migongano ya sheria ambapo ammewasihi wabunge kuangalia namna bora  ya kutunga sheria zinazokinzana.

Aidha, amesema rasilimali za misitu na nyuki huchangia asilimia 3.3 ya pato la Taifa, asilimia 5.9 ya mapato yatokanayo na biashara ya nje, na ajira takribani milioni 3 za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja. 

Pamoja na faida hizo, hifadhi za wanyamapori na misitu ni muhimu kwa mifumo ikolojia ikiwa ni pamoja na uhifadhi wa bioanuai, kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, hewa safi na kuhifadhi vyanzo vya maji.

Ameongeza kuwa Sekta hizi zinakabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo, ujangili, uvunaji haramu wa mazao ya misitu, uchimbaji haramu wa madini, uvamizi wa maeneo ya hifadhi kwa ajili ya shughuli za kulisha mifugo, kilimo na makazi na mioto haramu.