Wednesday , 16th Jan , 2019

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola ametengua uteuzi wa Makamanda wa Polisi katika mikoa 3 ya kipolisi kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo makamanda hao kushindwa kutekeleza majukumu yao.

Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola .

Waziri Kangi Lugola ametoa uamuzi huo akiwa Jijini Dodoma, ambapo ametengua uteuzi wa makamanda wa polisi wa mikoa mitatu akiwemo Salum Hamduni aliyekuwa Ilala, kwa kosa la kushindwa kusimamia mianya ya rushwa na utoaji wa dhamana kwa watuhumiwa.

Kamanda mwingine aliyetenguliwa kwenye nafasi yake ni Kamanda wa Polisi Mkoa wa Temeke, Emmanuel Lukula ambaye naye ametenguliwa kwa makosa hayo ya kushindwa kusimamia mianya ya rushwa na utoaji wa dhamana.

Akitangaza uamuzi huo mbele ya waandishi wa habari, Waziri Lugola ameeleza pia kumtengua kwenye nafasi yake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Ramadhani Ng'azi.

Aidha Waziri huyo amemtaka Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani, Fortunatus Muslimu kujitafakari na kujipima kama anatosha katika nafasi hiyo.