ACT-Wazalendo yatoa msimamo kwa wabunge wao

Jumapili , 8th Nov , 2020

Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Zuberi Kabwe amesema, wananchi wasitegemee kuwaona wabunge wa chama hicho bungeni na chama hicho kwa sasa hakiwazi suala la ruzuku au wabunge wa viti maalum.

Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Zuberi Kabwe.

Zitto amesema hayo leo Novemba 8, 2020  wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi za chama hicho, Magomeni jijini Dar es Salaam, ambapo amesema zaidi ya wanachama 169 nchi nzima wamekamatwa katika siku ambazo zimepita na bado wanaendelea kukamatwa.

Kwetu sisi hapakuwa na uchaguzi na kuna taratibu zinaendelea kufanywa ndani ya chama kwa wale waliotangazwa kushinda, lakini msitegemee kuona wabunge  waliotokana na ACT-Wazalendo bungeni”, amesema Zitto.

Hakuna jambo ambalo ni muhimu zaidi ya uhai wa watu, kiongozi mwenzangu (Mazrui) sijui anaendeleaje, sasa hivi siwazi ruzuku, viti maalum wala chochote, nachowaza ni damu ya wanachama wangu na uhai wa viongozi wangu”, ameongeza Zitto.

Katika uchaguzi Mkuu wa Oktoba 28, kati ya majimbo 264, ACT-Wazalendo ilijipatia majimbo manne ya Pemba-Zanzibar.