Namthamini imeendelea kuwa jukwaa muhimu la kutetea heshima, usawa na fursa kwa wasichana nchini Tanzania toka ilivyoanzishwa mwaka 2017 na EATV LTD kama kampeni ya uhamasishaji.
Kampeni hii ya Namthamini sasa imekuwa nembo muhimu inayotambulika kitaifa, ikilenga kukabiliana na changamoto ya hedhi kwa kuzingatia ustawi na ushiriki wa jamii katika kulinda heshima ya mtoto wa kike.
Kwa kuzingatia uzoefu uliopatikana kutokana na utekelezaji wa shughuli zake, maoni na mahitaji halisi ya wasichana walengwa, mwaka 2025 Namthamini ilifanya mabadiliko kutoka kampeni ya msimu wa utoaji taulo za kike na kuwa programu endelevu ya afya na usafi wa hedhi, inayotekelezwa mwaka mzima kwa kuzingatia miongozo ya Kitaifa ya Afya na Usafi wa Hedhi (MHH).
Mabadiliko haya yanaonesha kuwa heshima ya hedhi haiwezi kushughulikiwa kwa mifumo ya muda mfupi kwani wasichana hupitia mzunguko wa hedhi kila mwezi hivyo haki yao ya kupata elimu, kujiamini na kuishi kwa usalama, inapaswa kulindwa na kuimarishwa kwa misingi endelevu.
Namthamini inatoa shukrani za dhati kwa washirika wake wote ambao ni wafadhili, watu waliojitolea, wafanyakazi na wananchi kwa ujumla kwa mchango na ushirikiano unaoendelea. Umoja huu umeiwezesha Namthamini kukua kutoka wazo la awali na kuwa programu yenye mchango chanya na wa kudumu katika jamii.
'Unapomuinua mtoto mmoja wa kike, umeinua jamii nzima'
#Namthamini
#NasimamaNaye















